Dar es
Salaam. Wakati wasanii wengine wakifanya juhudi kuhakikisha wanasafiri kwenda
nje ya nchi kwa ajili ya kutengeneza video za nyimbo zao,, mwimbaji mwenye
sauti ya kuvutia, Bernard Paul maarufu ‘Ben Pol’ amesema kuwa hana mpango wa
kutengeneza video nje ya Tanzania.
Ben Pol
amesema licha ya video zake nyingi kuwa amezifanyia hapa nchini, lakini
zimefanikiwa kuonyeshwa katika vituo mbalimbali vya televisheni Afrika Kusini
na Afrika Mashariki kwa jumla.
“Iwapo
nitataka kutengeneza video kali ya kimataifa, nitamchukua mwongozaji kutoka nje
na kumleta hapa Tanzania,” hivi ndivyo anavyosema.
Anasema
kuwa ndani ya Tanzania kuna vivutio vingi anavyoamini akimchukua mwongozaji
mwenye vifaa vya kutosha vya kimataifa, ataweza kutengeneza video yenye ubora.
“Unapomchukua
mwongozaji kutoka nje na kumleta hapa, bila shaka itampa umakini mkubwa hata
yeye mwenyewe, hivyo kufanya mambo makubwa zaidi ya afanyavyo akiwa huko. Hapa
kwetu tuna vivutio vingi , maeneo yanayovutia kuna Lushoto, Arusha, Zanzibar,
Bagamoyo na mengine yanayoweza kutumika kwa shughuli hii na ukaushangaza
ulimwengu,” anasema Ben Pol.
Anasema
kuwa bado anahisi anao wajibu wa kuutangaza utalii wa ndani kupitia kazi yake
ya muziki.
“Nina
wajibu na jukumu la kuwa balozi mzuri nyumbani kwetu. Najua labda watu wa nje
wangependa kuona vitu vya nyumbani, ninapojitangaza kwamba mimi ni mwanamuziki
kutoka Tanzania, hata kwenye kazi zangu waone mazingira ya nchi yangu,”
anasema.
Je, hiyo ni sababu pekee ya uamuzi wake kufanyia kazi
zake Bongo?
Ben Pol
anaeleza kuwa, anapoona kazi zake zinatumika na kuombwa na watu wengi waishio
nje ya nchi, hufarijika kwani inaonyesha inaeleweka.
“Najua
kazi yangu inaeleweka, kwa watu wanaoijua lugha ninayoimba, hata kwa wale ambao
Kiswahili kwao ni mtihani. Napokea pongezi nyingi, mfano wimbo wa ‘Jikubali’ ni
kati ya kazi zangu zilizonipa umaarufu mkubwa nje ya nchi na ndiyo wimbo
uliopigwa zaidi nje kuliko kazi zangu zote,” anasema Ben Pol.
Kuhusu
usimamizi wa kazi zake Ben Pol anasema kuwa kwa sasa kuna mtu wa karibu
anayemsaidia katika suala hilo. Anamtaja kuwa ni mshirika wake wa karibu na
wanasaidiana katika kazi za muziki, lakini hana meneja.
Anabainisha
kuwa kuna faida kubwa kwa msanii kuwa na usimamizi, lakini akasema bado kuna
uhaba wa mameneja wa kazi za wasanii na kwamba kwa walipo sasa, wengi hawana
ufahamu wa kazi zao.