Wiki iliyopita Nature alielezea ujio wa kundi jipya
la Wanaume Halisi baada ya kuvunjika kwa Kundi la Wanaume Family.
Wiki hii pamoja na mambo mengine, nguli huyo wa
muziki wa kizazi kipya anaeleza jinsi alivyopata wakati mgumu kutunga mashairi
na hali ya muziki ilivyo.
Anaeleza kuwa iliwachukua siku nyingi kutunga
mashairi la wimbo mmoja na kwamba walifanya hivyo ili zidumu, hivyo shairi moja
lilikuwa likimchukua hadi mwezi mzima kukamilisha kulitunga.
“Labda uwezo wetu ulikuwa mdogo, naona siku hizi mtu
anatunga nyimbo 12 kwa siku. Mimi huwa nashangaa sana, au msanii mchanga
anakwambia ana albamu nne ingawa inasikika kwa singo moja,”anasema Nature.
Anasema kuwa ugumu wa kazi hiyo ulimfanya hata augue
homa kila alipomaliza kutunga nyimbo za albamu, kutokana na uchovu uliotokana
na kuishughulisha akili bila kutaka kubugudhiwa. Nature anaeleza kuwa ilifikia
wakati alikwenda kushinda ufukweni mwa bahari ili kukimbia marafiki ambao
wangemsumbua wakati anatunga mashairi.
“Hakuna albamu niliyotunga bila kupata homa, hasa ya
‘Ugali’ ndiyo niliumwa sana, ndiyo sababu nikiona mtu ametunga nyimbo zaidi ya
10 kwa siku, namshangaa na kuona ana uwezo sana, “anasema Nature.
Nature anazungumzia utunzi wa sasa na mapokeo ya
mashabiki akisema kuwa watunzi wengi hurudia ujumbe kutokana na kukosa umakini
na kuiga, hivyo kutodumu na kuyeyuka mapema mioyoni mwa mashabiki.
Anafafanua kuwa wasanii wengi wa muziki kwa sasa
wanaamini wakiimba singo moja watakuwa matajiri kutokana na kuwaona baadhi ya
wanamuziki wamefanikiwa na wao kutamani hali hiyo, lakini matokeo yake
wanaboronga.
Anaitaja changamoto wanakumbana nayo wasanii kwa
sasa kuwa ni wanaojiita wadau wa muziki wa kizazi kipya kuwatumia vibaya
wasanii na wanang’amua wanatumiwa, hupotezwa katika sanaa.
Anasema hali hiyo imekuwa inawaondoa kwenye soko
wasanii mahiri kwa sababu watu wanaowaamini huwanyonya na kuwaacha hoi.
“Hapa nawataka wasanii wenzangu kuwa makini na watu
hawa wanaojifanya wanapenda kuendeleza muziki na wasanii kwani mwishowe
huwapoteza makusudi katika sanaa ili kujilinda wasionekane wabaya, “anasema.
Kuhusu kuwapo kwa studio nyingi za muziki ikiwamo ya
kwake ( Halisi Recods), Nature alisema kuwa zinaleta ushindani unaozaa kazi
bora.