Dar es Salaam. Aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa
Tabora, Kansa Mbarouk amejitokeza ‘kupimana kifua’ na Mwenyekiti wa chama hicho
taifa, Freeman Mbowe katika uchaguzi wa ndani unaotarajiwa kufanyika Septemba
14.
Mbarouk alirejesha fomu hizo makao makuu ya Chadema jana mchana
huku akikumbana na kizingiti cha kuzuiwa na walinzi kuingia ndani kurejesha
fomu akiwa pamoja na waandishi wa habari na hata alipotoka nje hakutakiwa
kuzungumza na waandishi hao karibu na jengo hilo.
Ili kuepusha vurugu, Mbarouk alitoka eneo hilo na kuanza
kuzungumza na waandishi wa habari kwa kusema, “Hili ambalo limenipata kwa
kuzuiwa nisipigwe picha wakati nikirejesha fomu nikiingia madarakani
nitahakikisha narejesha usawa ndani ya chama hiki na katiba inazingatiwa.”
Aliongeza, “Jambo la pili kulifanya nitahakikisha wanachama wote
ndani ya Chadema wanakuwa na haki sawa, hakuna atakayeonewa na atakayevunja
katiba kwa njia zozote zile atachukuliwa hatua kali, hakuna atakayekuwa juu ya
katiba ya Chadema.”
Juzi, Mbowe alikabidhiwa fomu na makada wa chama hicho na
kumtaka awanie tena kiti hicho, ombi ambalo alilikubali na kufungua milango kwa
wanachama wengine ‘kupimana naye kifua’.
“Nafasi bado ipo, anayetaka kupima kifua na mimi ajitokeze. Tena
nawaomba viongozi wangu msizuie fomu kwa anayetaka,” alisema Mbowe ambaye
ameongoza chama hicho kwa vipindi viwili vya miaka mitano mitano.
Mbarouk alisema, kulingana na katiba ya chama Mbowe amemaliza
muda wake wa uongozi na anatakiwa kukiachia kiti hicho kiongozwe na mtu
mwingine.
“Mimi nimekuwa mwenyekiti wa mkoa (Tabora) kwa kipindi cha miaka
10 nikaamua kuachia ili wengine waendeleze vivyo hivyo na Mbowe ameongoza kwa
miaka kumi anatakiwa kuachia ngazi, na hii ni nafasi yangu imewadia kuiongoza
Chadema kufika Ikulu 2015,” alisema Mbarouk.
Huku akisisitiza alisema, “Kauli aliyoitoa Mbowe ya kusema
anayetaka kujipima kifua naye ajitokeze ni ya kuwatisha wanachama wasijitokeze,
lakini mimi siwezi kutishika na ndiyo maana nimejitokeza kupimana naye kifua na
ninajua nitamshinda kwani katiba ikizingatiwa tu hawezi kunishinda.” Uchaguzi
huo utatanguliwa na wa Baraza la Vijana Taifa la Chadema, (Bavicha)
utakaofanyika Septemba 10 huku Septemba 11 ukifanyika wa Baraza la Wanawake
(Bawacha).
Hadi dirisha la urejeshaji fomu linafungwa jana saa 10.30 makada
mbalimbali walikuwa wamejitokeza kuwania nafasi hiyo miongoni ni Daniel Madiba
anayewania Mratibu Mhamasishaji taifa wa Bavicha na wakili wa Mahakama Kuu ya
Tanzania, Lutiger Haule nafasi ya Ujumbe wa Kamati Kuu kupitia Vijana. Haule
alisema anataka kuwatumikia vijana katika kupata haki zao na atatumia nafasi
hiyo kuwapigania kwa nguvu zote katika harakati za kusaka ukombozi wa pili
unaominywa na CCM.
Ushindani ndani ya Bawacha unatarajiwa kuwa kati ya Mbunge wa
Kawe, Halima Mdee, Mbunge Viti Maalum, Chiku Abwao na makada wengine, Lilian
Wasira na Sophia Mwakagenda kwa nafasi ya mwenyekiti.
Katika hatua nyingine, nafasi ya Naibu Katibu Mkuu Baraza la
Wanawake ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Bawacha), imeendelea kupata wagombea
baada ya Aisha Yusuf kuchukua fomu na kuirejesha kuwania nafasi hiyo.