Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(Chadema), Freeman Mbowe jana alikabidhiwa fomu na makada wa chama hicho na
kumtaka awanie tena kiti hicho, ombi ambalo alilikubali na kufungua milango kwa
wanachama wengine ‘kupimana naye kifua’.
“Nafasi bado ipo, anayetaka kupima kifua na mimi ajitokeze. Tena
nawaomba viongozi wangu msizuie fomu kwa anayetaka,” alisema Mbowe ambaye
ameongoza chama hicho kwa vipindi viwili vya miaka mitano mitano.
Makada wa chama hicho kutoka maeneo mbalimbali nchini
wakiongozwa na kada maarufu, Athuman Mzigo (Mapigo Saba) kutoka Kigoma,
walikutana na Mbowe na kuwasilisha maombi yao ya kumtaka awanie tena nafasi
hiyo.
“Kutokana na sifa za mwenyekiti wetu, tumechangishana Sh200 kila
mmoja hadi zikafika Sh50,000,” alisema Mapigo Saba huku akishangiliwa na makada
wenzake alioambatana nao na kuongeza:
“Tumemwomba mwenyekiti agombee nafasi hiyo kwa kuzingatia sifa;
kwanza anaijua vizuri idadi ya Watanzania na matatizo yao, pili anaungwa mkono
na watu wengi na amekisaidia chama kukua. Tulikuwa na madiwani 40 leo wamefika
500, wabunge watano leo 48. Halafu hana ubaguzi ndiyo maana ameunganisha vyama
vya upinzani na kuunda Ukawa (Umoja wa Katiba ya Wananchi).”
Huku akichomekea maneno ya lugha ya Kiha, Mapigo Saba alisema
kuwa maombi ya kumtaka Mbowe agombee pia yametolewa katika mikoa ya Rukwa,
Manyara, Iringa, Njombe, Jimbo la Same Magharibi, Zanzibar, Mwanza na
Kilimanjaro.
Hotuba ya Mapigo Saba ilifuatiwa na salamu kutoka kwa wazee wa
wilaya za Kinondoni, Ilala na Temeke, Baraza la Wanawake (Bawacha) na Baraza la
Vijana (Bavicha).
Akitoa salamu za Bavicha, mwenyekiti wa baraza hilo Njombe,
Emmanuel Masonga alisema Mbowe ni sawa na Joshua aliyemalizia kuwaongoza wana
wa Israel kuingia nchi ya Kanaani:
“Sisi Wakristo tunajua kuwa Mussa alianzisha safari ya Waisrael
kwenda Kanaani, ila hakuwafikisha. Kina Mtei (Edwin), Kimesera (Victor), Bob
Makani na wengineo walianzisha safari ya kwenda Ikulu, ila hawakutufikisha.
Mbowe ni sawa na Joshua atakayetufikisha Ikulu,” alisema Masonga.
Mwenyekiti wa Bawacha Taifa, Susan Lymo alimsifu Mbowe akisema
ameongeza hamasa ya wanawake kushiriki siasa katika chama hicho.
“Mwaka 2000, kulikuwa na mwanamke mmoja katika viti maalumu,
mwaka 2005 waliongezeka na kufikia sita na mwaka 2010 wamefikia 26. Mwenyekiti
pia ameufanya mwaka huu kuwa wa wanawake kitaifa na ameongeza hamasa ya
wanawake kushiriki siasa,” alisema Lymo.
Mbali na viongozi wa chama, alikuwapo pia Sheikh Rajab Katimba
kutoka Jumuiya na Taasisi za Kiislamu ambaye alimsifu Mbowe na kuomba agombee
tena nafasi hiyo.
SOURCE Mwananchi;