TANGAZA NA TAZAMA HABARI

FANYA BIASHARA YAKO IJULIKANE ZAIDII jivunie kua mwanafamilia wa tazama habari ! WEAPON FOUNDATION TANGAZA BIASHARA YAKO NASI ILI UWAFIKIE WATU WENGI ZAIDI TUNAKUSHUKURU KWA KUA MWANAFAMILIA WA TAZAMA HABARI

Tuesday, August 26, 2014

Rais JK ampa kazi ngumu Waziri Maghembe

 Rais Jakaya Kikwete amemwagiza Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe kwenda kuwaeleza wananchi wa Mji wa Dumila wilayani Kilosa sababu za kusuasua kwa utekelezaji wa mradi wa maji na lini tatizo la kukosekana kwa huduma hiyo litapatiwa ufumbuzi.

Pia ametoa agizo kama hilo kwa watendaji wa Kitengo cha Maafa katika Ofisi ya Waziri Mkuu, ambao kwa upande wao, wametakiwa kuwaeleza walioathiriwa na mafuriko yaliyotokea mapema mwaka huu, kiini cha kasi ndogo ya ujenzi wa makazi yao.
Rais Kikwete alitoa maagizo hayo juzi usiku alipokuwa akizungumza na wananchi wa Dumila baada ya kufungua barabara mpya ya Dumila-Ludewa wilayani Kilosa, yenye urefu wa kilometa 45 iliyojengwa kwa Sh48.69 bilioni.
Alisema tatizo la maji katika mji huo ni la muda mrefu na kwamba inashangaza kusikia kuwa hata utekelezaji wa mradi ambao ungemaliza kero hiyo kwa wananchi, umekuwa wa kusuasua kwa sababu ambazo hazijulikani.
Kwa sasa sehemu kubwa ya wananchi wa mji huo ulioko katika Barabara Kuu ya Morogoro- Dodoma, wanategemea zaidi maji ya kununua yanayopatikana kutoka katika vyanzo visivyokuwa vya uhakika.
Kwa mujibu wa baadhi ya wananchi, dumu moja la maji hayo, linauzwa Sh500.
“Mwaka 1993 nikiwa waziri nilifanya mkutano hapa (Dumila) wakati huo Mbunge wa Kilosa alikuwa marehemu Shaweji (Abdallah), mtu mmoja alisimama na kumtaka mbunge aeleze kwa nini tatizo la maji halipatiwi ufumbuzi.
“Najua hizo zilikuwa ni hasira, lakini fikiria nimekuwa waziri hadi sasa nimekuwa Rais, tatizo bado lipo. Sasa nasema hivi, namwagiza Waziri wa Maji achague ama Jumamosi au Jumapili ya wiki ijayo, aje hapa awaelezeni lini tatizo hili litakwisha. Haiwezekani niondoke madarakani kabla tatizo la maji Dumila halijapatiwa ufumbuzi,” alisema Rais Kikwete.
Pia alielezea kutoridhishwa kwake na kasi ndogo ya ujenzi wa makazi ya watu waliokumbwa na mafuriko na kwamba hatua lazima zichukuliwe kuharakisha ujenzi wa makazi hayo ili wananchi hao waweze kuishi maisha ya kawaida.
“Nawaagiza watendaji wa Kitengo cha Maafa katika Ofisi ya Waziri Mkuu, nao waje waseme kwa nini kasi ya ujenzi wa makazi ya watu walioathiriwa na mafuriko ni ndogo,” alisema.
Kuhusu barabara aliyoifungua, Rais Kikwete alisema itakuwa kichocheo kikubwa cha maendeleo ya wananchi wa Dumila na maeneo mengine ya jirani.
“Shabaha yetu ni kuona kuwa barabara hii inatoka hapa Dumila-Ludewa-Kilosa hadi Mkata ili kuchochea kasi ya maendeleo,” alisema na kumpongeza Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli kwa ujenzi wa barabara nchini.

source Mwananchi;