Dar es Salaam. Kiongozi wa Jumuiya za Uamsho na Mihadhara ya
Kiislamu Zanzibar (Jumiki), Sheikh Farid Hadi Ahmed amemuomba Rais kuunda tume
itakayowahusisha watu kutoka Tanzania Bara, Zanzibar, wanasheria na madaktari
ili waweze kuchunguza afya zao.
Sheikh Farid aliyaeleza hayo jana muda mfupi baada ya mawakili
wa Serikali Peter Njike na George Barasa kuiomba mahakama kubadilisha hati ya
mashtaka ya ugaidi iliyokuwa ikiwakabili na kumuunganisha Sheikh Mselem Ali
Mselem na mwenzake Abdallah Said Ali na kufanya idadi ya washtakiwa hao wa
ugaidi kufikia 22.
Farid alimueleza hakimu kuwa anacho cha kusema na akapewa
nafasi, kisha akadai kuwa Agosti 6 na 21, 2014 walifika mahakamani hapo na
kueleza matatizo, madhila na unyama waliofanyiwa na polisi na siyo magereza.
Alidai kuwa gerezani wanaishi vizuri kwa kufuata sheria
isipokuwa suala la matibabu ambapo aliongeza kuwa uwezo wa bajeti yake ni mdogo
hivyo wanashindwa kuwatibia jambo ambalo linasababisha waagize dawa nje wakati
ugonjwa huwa hausubiri.
“Watu wameingia gerezani wanaumwa wanavuja hadi usaa kutokana na
kipigo walichopewa na polisi hivyo tunamuomba Rais aunde tume kutufanyia
uchunguzi wa afya zetu,”alisema na kuongeza;
“Sisi tunachodai siyo uchochezi ninayoeleza polisi wapo
wameyasikia tumekamatwa na kushtakiwa Tanganyika kwani Zanzibar siyo nchi.”
Hakimu Hellen Liwa alimueleza kuwa yeye anachojua wote ni
Watanzania na suala la Muungano wengine wanauamini na wengine wanataka ukazikwe
Butiama.
Hakimu alimtaka aandike kwa maandishi malalamiko yake ili waweze
kuyapeleka sehemu husika na kuiahirisha kesi hiyo hadi Septemba 17, 2014.
Baada ya kutolewa kwa ombi hilo, Hakimu Hellen Liwa alikubaliana
na ombi hilo na mawakili hao waliwaunganisha washtakiwa hao na kuwasomea
mashtaka manne mapya.
Mawakili wa Serikali, Njike na Barasa jana walidai mbele ya
Hakimu Liwa kuwa washtakiwa hao walijihusisha na mashtaka yakiwamo ya kula
njama na kuwaingiza watu kushiriki vitendo vya ugaidi kinyume na kifungu cha
27(c) cha Sheria ya Kuzuia Ugaidi ya mwaka 2002.
Njike alidai mahakamani hapo kuwa washtakiwa hao kwa pamoja
waliwaingiza nchini Sadick Absaloum na Farah Omary ili kutenda makosa ya
ugaidi.
Sheikh Farid na Mselem kwa makusudi wanadaiwa kutoa msaada kwa
Absaloum na Omary ili waweze kushiriki katika vitendo vya kigaidi.